Kwa mujibu wa Kitengo cha tarjama cha Shirika la Habari la Hawza, Hussein al-Nimr aliyasema hayo katika hafla ya kumbukumbu ya mwaka wa kwanza wa mashahidi wa “Njia ya Quds” iliyofanyika katika mji wa Halaniyah, akibainisha kwamba: “Jamii ya muqawama katika kila uchaguzi imethibitisha kuwa ni jamii yenye nguvu, jasiri na isiyoshindwa, ambayo kamwe haitasalimu wala kuacha mapambano yake.”
Ameongeza kuwa: “Uchaguzi wa bunge ujao utakuwa ni hatua muhimu katika kuimarisha upya imani na uaminifu wa wananchi kwa chaguo la muqawama.”
Alisema kuwa katika uchaguzi wa serikali za mitaa uliopita, kulikuwepo na changamoto kubwa, lakini wananchi walithibitisha uungaji mkono wao wa dhati kwa muqawama, na kura zao zilikuwa kama risasi dhidi ya wale wote waliotaka kudhoofisha chaguo lao.
Hussein al-Nimr aliendelea kusema: “Kwa wale wanaoota kwamba wataweza kutushinda kupitia masanduku ya kura, tunawaambia: uchaguzi unakuja, na mtashuhudia nguvu ya jamii hii kubwa.”
Mjumbe huyo wa Hizbullah pia alionya kwamba “Kwa wale wanaotamani kuondosha orodha ya wagombea wa muqawama katika eneo la Baalbek–Hermel, tunasema: yeyote atakayejiorodhesha katika orodha zinazolenga kupambana na muqawama au zinazotaka kuondoa silaha zake, ataonekana kama msaliti wa damu za mashahidi na atatengwa na jamii, kwani miji yetu haikubali vibaraka wala watu dhaifu wa moyo.”
Mwisho, Hussein al-Nimr alisema kwa kujiamini kuwa: “Tuna hakika kuwa watu wetu watajitokeza kwa wingi katika uchaguzi ujao, na kura zao zitakuwa muhuri wa kuthibitisha mafanikio na ushindi wa harakati yetu.”
Maoni yako